A great place to access the latest news and information.

Breaking

Post Top Ad

Your Ad Spot

Thursday, May 13, 2021

Waziri Ummy Mwalimu aitaka jamii kuheshimu kazi za wauguzi nchini

Makundi mbalimbali katika jamii yametakiwa kuheshimu na kutambua kazi za huduma ya afya zinazofanywa na wauuguzi nchini ili kuondoa tabia ya kuwadhalilisha na wakati mwingine kuwatukana katika maeneo yao ya kazi.

Hayo yamesemwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Mhe. Ummy Mwalimu katika maadhimisho ya Siku ya Wauguzi Duniani ambayo yamefanyika kitaifa kwenye viwanja vya Kwaraa, mjini Babati, mkoani Manyara. Kauli mbiu ya mwaka huu ni ‘Wauguzi, Sauti inayoongoza Dira ya Huduma ya Afya.’

Waziri Ummy Mwalimu amesema kazi ya uuguzi ni fani muhimu ambayo inapaswa kuheshimiwa na jamii kwa sababu kazi wanayofanya ni kuokoa maisha ya wananchi mara wanapokwenda hospitali kupata huduma ya afya.

“Nimeongea na wauguzi wa Muhimbili, MOI, JKCI na wale wa hospitali za rufaa, wote wamenieleza shida kubwa inayowakabili ni maumivu ya mgogo kutokana na kazi kubwa wanayofanya, hivyo natambua changamoto zenu na nitazifanyia kazi,” amesema Waziri Mwalimu.

Mkurungezi wa Mafunzo wa Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dkt. Saitori Laizer amesema wauguzi ni watumishi muhimu katika sekta ya afya kwani wamekuwa wakitumia saa nyingi katika sehemu kazi na kwamba huwezi kutaja mafanikio katika sekta ya afya, bila kuwataja wauguzi.

Dkt. Saitori amewataka wauguzi kutumia fursa mbalimbali zinazojitokeza katika sekta ya afya, mfano nafasi za kujiendeleza kielimu ambazo zimekuwa zikitolewa na wizara ya afya.

Katika hatua nyingine, Afisa Muuguzi wa Hospitali ya Taifa Muhimbili Mloganzila, Bw. Wilson Fungameza ameshukuru uongozi wa Hospitali ya Taifa Muhimbili Upanga na Mloganzila kwa kumuunga mkono katika ubunifu wa kutengeneza kifaa cha kusaidia watoto wenye matatizo ya upumuaji pamoja na kuandika kitabu cha kusaidia wauguzi katika utoaji wa huduma za afya kwa wagonjwa mbalimbali.

Naye Afisa Muuguzi wa Hospitali ya Taifa Muhimbili Upanga, Bi. Leonia Shirima amemshukuru Waziri wa TAMISEMI, Mhe. Mwalimu kwa kupokea changamoto mbalimbali za wauguzi walizozitoa katika maadhimisho hayo.

Awali, wauguzi hao walikumbushwa kuzingatia kiapo chao na kufanya kazi kwa bidii, kujitoa, kuzingatia weledi wakati wa kuwahudumia wagonjwa kwa kuwa muuguzi ni mtu wa kwanza anayekutana na mgonjwa pindi anapofika hospitalini kupata mabibu.

Pia, kabla ya kilele cha maadhimisho hayo, wauguzi wa Hospitali ya Muhimbili Upanga na Mloganzila walishiriki katika kutoa elimu ya afya kwa wanafunzi wa Shule ya Sekondarii Malamba-mawili, Manispaa ya Ubungo jijini Dar es Salaam.

Mwenyekiti wa Chama cha Wauguzi Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), Bw. David Mpayuke alisema lengo la kutoa elimu kwa wanafunzi ni kuwahamasisha kujiunga na fani ya uuguzi pamoja na kuboresha afya ya jamii, afya ya akili, afya ya uzazi, usafi na huduma ya kwanza shuleni.



Afisa Muuguzi wa Muhimbili Mloganzila, Bw. Wilson Fungameza akikabidhiwa cheti cha mfanyakazi bora kitaifa kutokana na ubunifu wa kutengeneza kifaa cha kusaidia watoto wenye matatizo ya upumuaji pamoja na uandishi wa nakala mbalimbali za vitabu vya wauguzi kuhusu huduma za afya.




Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Mhe. Ummy Mwalimu ambaye ni mgeni rasmi akizungumza na wauguzi mbalimbali wakiwamo wa Hospitali ya Muhimbili Upanga na Mloganzila katika viwanja vya Kwaraa, mjini Babati mkoani Manyara ambako wauguzi hao wameadhimisha Siku ya Wauguzi Duniani.
Baadhi ya wauguzi kutoka mikoa mbalimbali nchini wakimsikiliza Waziri wa TAMISEMI, Mhe. Ummy Mwalimu katika viwanya vya Kwaraa, mjini Babati mkoani Manyara.

Wauguzi kutoka hospitali mbalimbali nchini wakiapa mbele ya mgeni rasmi, Waziri wa TAMISEMI, Mhe. Ummy Mwalimu. Mkurugenzi wa Uuguzi wa Hospitali ya Taifa Muhimbili Upanga, Bi. Zuhura Mawona na Kaimu Mkurugenzi Msaidizi wa Uuguzi Hospitali ya Taifa Muhimbili Mloganzila. Bi. Redemta Matindi ni baadhi ya washiriki walioapa katika kuadhimisha Siku ya Wauguzi Duniani.

Afisa Muuguzi wa Hospitali ya Taifa Upanga, Bi. Martha Bruckman akimpatia kipeperushi mmoja wa wananchi wa mjini Babati, mkoani Manyara aliyefika katika banda la Muhimbili Upanga na Mloganzila kupata elimu ya afya kuhusu magonjwa mbalimbali.

Mkazi wa Babati, mkoani Manyara Bw. Fredrick Suleiman (kulia) akimsikiliza Afisa Muuguzi wa Hospitali ya Taifa Muhimbili Upanga, Bw. David Mpagike kuhusu elimu ya afya ya akili.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages