WAZIRI
wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, Mheshimiwa
Dkt. Suleiman Jafo (Mb) ameunda Kamati ya Kitaifa ya watu 11 kwa ajili
ya kuchunguza chanzo cha uchafuzi wa maji ya Mto Mara.
Akizungumza
leo Machi 12, 2022 baada ya kutembelea Mto Mara katika eneo la Kirumi
na kupokea taarifa kutoka kwa viongozi, wananchi na wataalamu,
Mheshimiwa Jafo ameitaka kamati hiyo kufanya uchunguzi wa maji ya mto
huo na kutoa taarifa ndani ya kipindi cha siku saba kuanzia leo.
Mheshimiwa
Jafo, amesema mbali na kufanya uchunguzi wa maji ya Mto Mara pia,
ifanye uchunguzi wa maji yote kandokando ya mto huo ili kuona kama kuna
uchafuzi wa namna hiyo na kutoa mapendekezo ya kitaalam ili kukabiliana
na uchafuzi huo katika Mto Mara.
Mheshimiwa
Jafo amesema kuwa, Mwenyekiti wa Kamati hiyo ni Prof. Samwel Manyele,
kutoka Idara ya Uhandisi wa Kemikali na Madini, Chuo Kikuu cha Dar es
Salaam (UDSM) na Katibu wa Kamati hiyo ni Dkt. Samuel G. Mafwenga,
Mkurugenzi Mkuu, Baraza la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC).
Wajumbe
wa kamati hiyo ni pamoja na Dkt. Kessy F. Kilulya, Mkuu wa Idara ya
Kemia, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Dkt. Charles Kasanzu, kutoka
Idara ya Jiolojia, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Bwana Daniel
Ndio, Mkurugenzi wa Udhibiti na Usimamizi wa Kemikali, Mamlaka ya Mkemia
Mkuu wa Serikali (GCLA) na Bwana Renatus Shinhu, Mkurugenzi wa Bonde,
Mamlaka wa Bonde la Maji Ziwa Victoria.
Mheshimiwa
Jafo amewataja wajumbe wengine kuwa ni Baraka Sekadende, Mkurugenzi wa
Kituo, Taasisi ya Utafiti wa Samaki (TAFIRI), Mwanza, Dkt. Neduvoto
Mollel, kutoka Mamlaka ya Afya ya Mimea na Usimamizi wa Viatilifu
(TPHPA), Afisa kutoka Ofisi ya Rais Ikulu, Bwana Yusuf Gobe Kuwaya
kutoka Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mara na Faraja Ngelageza, Mkurugenzi
Msaidizi Bioanuai, kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais.
Mheshimiwa
Jafo amesema kutokana na uchafuzi huo, maji yamebadilika rangi, yanatoa
harufu na samaki aina ya sato wamekuwa wanakufa na kuelea katika mto
huo.
Mheshimiwa
Jafo amewataka wananchi, Serikali na wadau wote kutoa ushirikiano wa
kutosha kwa Kamati hiyo katika kipindi chote watakachokuwa wanafanya
uchunguzi wa jambo hilo.
Pia,
Mheshimiwa Jafo ameitaka Mamlaka ya Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini
(RUWASA) kutafuta mbadala wa upatikanaji wa maji kwa wananchi waliopo
kandokando ya mto Mara wakati uchunguzi ukiwa unaendelea kufanywa juu ya
jambo hilo.
Mkutano
wa Mheshimiwa Jafo ulihudhuriwa na Mkurugenzi Mkuu wa NEMC, Mkemia Mkuu
wa Serikali Dkt. Fidelis Mafumiko, Wakuu wa Wilaya za Rorya, Tarime na
Butiama, wataalamu kutoka taasisi mbalimbali zinazohusiana na Maji,
Mazingira na Barabara.
Juma
Peter ni mkazi wa eneo la Kirumi ambapo amesema, hatua ya Serikali
kuchukua hatua za haraka juu ya Jambo hilo, inamanufaa makubwa kwa
wananchi ambao wamepatwa na hofu juu ya hali hiyo.
"Hali
hii imetutisha sana mto Mara kuchafuka na viumbe wakiwemo samaki kufa
na kuelea juu, lakini naishukuru Serikali kufika na kuchukua hatua
ambazo zinatija kwa wananchi na maisha yao kwa hakika serikali inatujali
wananchi wake,"amesema Peter.
No comments:
Post a Comment