RAIS
wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Hussein Ali
Mwinyi amesema kwamba ili kuweza kutekeleza mipango ya maendeleo kwa
ufanisi katika sekta za viwanda, utalii, ujenzi wa miundombinu na kutoa
huduma bora za afya na elimu ni lazima kuwepo na huduma ya maji safi na
salama ya uhakika.
Rais
wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe.Dkt.Hussein Ali
Mwinyi akihutubia na kuufungua Mkutano Mkuu wa Uwekezaji wa Sekta ya
Maji Barani Afrika uliofanyika Zanzibar katika ukumbi wa Hoteli ya Melia
Mkoa wa Kaskazini Unguja leo Machi 11,2022. Uliowashirikisha wadau
mbalimbali kutoka ndani na nje ya Tanzania.(Picha na Ikulu).
Rais
Dkt. Mwinyi aliyasema hayo leo Machi 11, 2022 wakati akifungua mkutano
wa Wadau wa Ngazi ya Juu wa Mashirikiano katika Uwekezaji wa Sekta ya
Maji Kusini mwa Afrika (GWPSA), uliofanyika katika Hoteli ya Melia,
Kiwengwa, Mkoa wa Kaskazini Unguja ukiongozwa na Mwenyekiti wake Rais
Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete.
Katika
maelezo yake, Rais Dkt.Mwinyi alisema kuwa, anaamini kwamba mkutano huo
utatoa elimu na uzoefu kutoka kwa wataalamu mbali mbali waliojumuika
pamoja ili Zanzibar nayo iweze kuimarisha upatikanaji wa maji safi na
salama kwa wananchi.
Amesema
kuwa,mkutano huo pia umekuja wakati muafaka ambapo kutokana na
mabadiliko ya hali ya hewa sehemu nyingi za ukanda wa Afrika Mashariki
na Kusini kumekuwa na changamoto kubwa ya upungufu wa maji.
Rais
Dkt. Mwinyi alisema kuwa, amekuwa akijiuliza siku masuala mengi kuhusu
mbinu na njia bora za kufanya ili kuweza kuondokana na changamoto ya
upatikanaji wa maji safi na salama hapa Zanzibar ambayo bado inawakumba
wananchi katika maeneo mbali mbali Unguja na Pemba.
“Kwa
hapa Zanzibar nimekuwa nikipokea taarifa za kuendelea kukauka visima
mbali mbali vinavyotumiwa na wananchi,”alisema Dkt.Mwinyi.
Aidha,
alieleza kufarijika kwake na ufunguzi wa mkutano huo ulioambatana na
uzinduzi wa Mpango wa Miaka mitano ya uwekezaji katika sekta ya Maji
Zanzibar, ambapo utekelezaji wake utafanywa baina ya kipindi cha mwaka
2022 hadi 2027.
Alieleza
matumaini yake kwamba maazimio yatakayopitishwa katika mkutano huo
yatakuwa na mchango mkubwa katika kufanikisha malengo ya kuanzishwa
Programu hiyo pamoja na kuzitafutia ufumbuzi changamoto mbalimbali
zilizopo katika sekta ya maji.
Rais
Dkt.Mwinyi alitoa pongezi kwa Mwenyekiti wa Ushirikiano wa Maji Duniani
(GWP) Kusini mwa Afrika, Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, Rais Mstaafu wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuridhia mkutano huo kuja kufanyika
hapa Tanzania.
Pamoja
na hayo, Rais Dkt.Mwinyi alisema kuwa, Serikali ya Mapinduzi ya
Zanzibar inaendelea kufanya juhudi mbalimbali za kuimarisha sekta ya
maji hapa Zanzibar ili kuhakikisha kuwa wananchi wanapata huduma za maji
safi na salama kwa uhakika.
Alieleza
mategemeo yake kwamba mkutano huo utatoa fursa ya kujifunza kutoka kwa
walioshiriki namna bora ya kuimarisha upatikanaji wa huduma za maji
safi na salama pamoja na njia bora za upatikanaji wa uwezeshaji katika
sekta hiyo kutoka katika vyanzo vya Kitaifa na Kimataifa ikiwemo sekta
binafsi.
Sambamba
na hayo, Rais Dkt.Mwinyi alieleza namna Serikali ya Mapinduzi ya
Zanzibar ilivyoweka mikakati yake katika kuimarisha Uchumi wa Buluu
ambao ndio Dira ya uchumi wa Zanzibar hivi sasa pamoja na kueleza sekta
zilizomo ndani yake.
Alieleza
kwamba mikutano ya Taasisi ya Ushirikiano ya Maji Kusini mwa Afrika
(GWPS) ambao hufanyika kila baada ya miaka miwili kwa lengo la kufahamu
mafanikio yaliyopatikana katika kuimarisha sekta ya maji kwa nchi
wanachama pamoja na changamoto zilizopo katika kuimarisha sekta ya maji.
Rais
wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe.Dkt.Hussein Ali
Mwinyi akionesha Kitabu cha Mpango wa Miaka Mitano ya Uwekezaji katika
Sekta ya Maji Zanzibar, baada ya kuzindua mpango huo, wakati ufunguzi wa
Mkutano Mkuu wa Uwekezaji wa Sekta ya Maji Barani Afrika, uliofanyika
katika ukumbi wa Hoteli ya Melia Kiwengwa na (kulia kwa Rais) Rais
Mstaafu wa Tanzania Mwenyekiti wa Taasisi ya (GWPSA), Mhe.Dkt.Jakaya
Mrisho Kikwete na (kushoto kwa Rais) Waziri wa Maji,Nishati na Madini
Zanzibar, Mhe.Shaib Hassan Kaduara.(Picha na Ikulu).
Amesema
kwamba, lengo la mkutano huo ni kupanga na kujadili mbinu mbalimbali za
kukabiliana na mabadiliko ya hali ya hewa na tabia nchi ili kuimarisha
upatikanaji wa maji safi na salama pamoja na kuyaweka mazingira katika
hali ya ubora zaidi.
Mapema
Rais mstaafu wa Awamu ya Nne wa Serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa
Tanzania ambae pia ni Mwenyekiti wa Mkutano huo,Dkt. Jakaya Mrisho
Kikwete, alisema kwamba kwa kiasi kikubwa changamoto ya maji katika bara
la Afrika husabanishwa na mabadililo ya tabia ya nchi.
Alisema
ili kuondokana na tatizo hilo ni lazima miradi mikubwa ya maji
itekelezwe kwa haraka ili kukabiliana na changamoto hiyo katika nchi za
Afrika.
Aidha,
alisema wana programu ambayo imepitishwa katika mkutano wa 34 wa Afrika
na upo mfumo uliotengenezwa ili kufikia malengo ya uanzishwaji wa
program ya maji Afrika.
Alisema
kuwa, lazima viongozi wa nchi za Afrika wawe na mkakati wa pamoja kutoa
kipaumbele kuongeza kasi ya upatikanaji wa maji katika mataifa yao.
Rais
wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe.Dkt.Hussein Ali
Mwinyi na (kulia kwa Rais) Rais Mstaafu wa Tanzania na Mwenyekiti wa
Taasisi ya (GWPSA), Mhe.Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete na (kushoto kwa Rais)
Waziri wa Maji,Nishati na Madini Zanzibar Mhe. Shaib Hassan Kaduara,
wakifuatilia mada ikiwasilishwa wakati wa mkutano huo Mkuu wa Uwekezaji
wa Sekta ya Maji Barani Afrika uliofanyika Zanzibar katika ukumbi wa
Hoteli ya Melia Kiwengwa Mkoa wa Kaskazini Unguja leo.(Picha na Ikulu).
Mwenyekiti
huyo alimuhakikishia Rais Dkt.Mwinyi kwamba taasisi hiyo anayoiongoza
itaendelea kuziunga mkono juhudi za Rais Dkt.Miwnyi katika kuhakikisha
changamoto ya upatikanaji wa huduma ya maji inapatiwa ufumbuzi hapa
Zanzibar.
"Nchi
za Afrika lazima ziweke mazingira mazuri ya uwekezaji ili kuvutia sekta
binafsi kuwekeza zaidi kwenye maji, jambo litakalosaidia kuondoa hadha
ya huduma hii muhimu kwa ustawi wa wananchi,"alisema.
Naye
Mkurugenzi Mkuu Mtendaji wa Shirika la Maendeleo la Umoja wa Afrika,
Ibrahim Assane Mayaki, akizungumza kwa njia ya mtandao, alisema kuna
mahitaji makubwa ya kuleta mabadiliko katika nchi za Afrika katika sekta
ya maji.
Alisisitiza
mashirikiano kwa nchi za Afrika katika kulenga kutekeleza matarajio ya
watu wa Afrika sambamba na kulinda vianzio vyake vya maji ili kuona
wananchi wanapata huduma hiyo.
Mkuu
wa Mkoa wa Kaskazini Unguja, Ayoub Mohammed Mahmoud, alisema hali ya
ubatikanaji wa maji katika mkoa inaridhisha kiasi lakini bado wananchi
wana uhitaji wa huduma hiyo hivyo ni vyema kwa wataalamu kuwa na
mazingatio ya upatikanaji wa huduma hiyo lakini pia juu ya kuitunza
rasimali hiyo kwa manufaa ya nchi.
Nao
viongozi wa Mashirika ya Kimataifa yakiwemo ya Umoja wa Mataifa
wakizungumza kwa njia ya mtandao walieleza umuhimu wa sekta ya maji na
kueleza namna watakavyounga mkono juhudi zitakazochukuliwa katika
kuhakikisha huduma hiyo inapatikana katika .
Katika
mkutano huo Rais Dkt. Mwinyi alizindua Mpango wa Miaka Mitano ya
Uwekezaji katika Sekta ya Maji Zanzibar pamoja na kutoa tunzo maalum kwa
wafadhili wa mkutano huo.
No comments:
Post a Comment