Na Mwandishi Wetu,Mtwara
KATIBU
wa Halmashuri Kuu ya CCM Taifa Itikadi na Uenezi, Shaka Hamdu Shaka
ametoa maagizo kwa Uongozi wa Bandari ya Mtwara ikiwemo kuhakikisha
bandari hiyo kuanza kutoa huduma za haraka ili kuzalisha ajira,
kuchochea uchumi wa Mtwara na nchi pia.
Pia ameitaka mamlaka hiyo
ya bandari kuweka mkakati thabiti wa kuitangaza bandari hiyo ili
wafanyabiashara na wawekezaji mbalimbali waijue na waitumie kuingiza na
kusafirisha mizigo yao.
Akitoa maagizo hayo leo, Septemba17
2021, Shaka akiwa Wilayani Mtwara ikiwa ni muendelezo wa ziara ya
wajumbe na sekretariet inayoongozwa na Katibu Mkuu Daniel Chongolo.
Amesema
pamoja na uwekezaji Mkubwa uliofanyika katika bandari hiyo wa
takribani bilioni 158.8 za kuboresha ni ajabu haitoi huduma kama
ilivyokusudiwa. "Sababu ikiwa ni urasimu na hata hujuma zinazofanywa na
baadhi ya watendaji wa kiserikali kwa kushirikiana na baadhi ya
wafanyabiashara wasio waaminifu," amesema Shaka
Amesema Chama
chao hakitakubali kuona utekelezaji wa ilani yao ya uchaguzi
unakwamishwa kwani kufanya hivyo ni kumkwamisha Rais Samia Suluhu
Hassan na kuchelewesha maendeleo ya wananchi na Taifa kwa ujumla.
"Haiwezekani
Rais Samia amemtuma Waziri Mkuu Majaliwa lakini baadhi ya watendaji
wasiwaminifu wamepuuza maagizo hayo kamwe CCM haitamvumilia yoyote
mwenye nia ovu ya kukwamisha jitihada za Rais Samia katika kuwaletea
maendeleo watanzania atakwama yeye,"amesema Shaka Mwenezi Taifa
Wakati
huo huo Shaka ameitaka Wizara ya Afya kuacha sinema za maonesho kwa
kutoa maelekezo na ahadi zisizotoa matokeo yanayopimika na kuonekana kwa
wananchi.
"Naitaka wizara ya Afya kueleza kama walimdanganya
Makamu wa Rais wa Tanzania Dkt Philip Mpango alipofika kuweka jiwe la
msingi mapema mwezi Oktoba katika Ujenzi wa hospital ya kanda Mtwara
inayogharimu takribani bilioni 15, ambapo walimwambia kuwa itakuwa
imeanza kutoa huduma lakini ajabu mpaka leo hakuna dalili hizo. "amesema
na kuongeza
"Sasa ni vizuri wabadilike waanze kuwa watendaji
badala ya kuwa wapiga maneno matupu...pamoja na kasi nzuri ya ujenzi
inayofanywa na mkandarasi ambaye ni shirika la Nyumba la Taifa, wizara
hiyo imekuwa kikwazo kikubwa katika kuhakikisha hospitali hiyi
inakamilika na kuanza kutoa huduma kwa wananchi,"amesema
No comments:
Post a Comment