Kiwavijeshi aina ya Fall Armyworm (FAW)
Wizara ya Kilimo Mifugo na Uvuvi imeanza jitihada za kuwakabili
Viwavijeshi wapya aina ya Fall Armyworm (FAW) wanaojulikana kitaalamu kama
Spodoptera Frugiperda ambao wametajwa kuwa na uwezo mkubwa kuharibu mazao
mbalimbali hususan mahindi ambayo ndio zao kuu la chakula nchini.
Imeelezwa kuwa Viwavijeshi hao wanapofika kwenye mazao hutoa kemikali
ambayo huweza kudanganya mmea kuwa unashambuliwa na magonjwa kama ukungu au
fangasi hivyo mmea unapohisi unashambuliwa na hayo magonjwa, hupunguza kinga
dhidi ya wadudu hao hatari na kuwa rahisi kushambuliwa.
Mkurugenzi Msaidizi wa Idara ya Maendeleo ya Mazao Wizara ya Kilimo
Mifugo na Uvuvi, Bwana Beatus Malema akizungumza wakati akifungua warsha ya
siku moja kujadili namna ya kukabiliana na mdudu aina ya Kiwavijeshi.
Mkutano ulikuwa na lengo la kujenga uelewa wa pamoja kwa ajili ya
kumkabili mdudu huyo aina ya Fall Armyworm (FAW) ambaye anashambulia mazao
mbalimbali nchini hususani zao la mahindi.
Alisema Athari ya viwavi jeshi haishii kuharibu majani ya mimea pekee,
wadudu hao wanapokula majani na kutengeneza sumu aina ya ‘firenide’ inayodhuru
mifugo inapokula majani yaliyoathiriwa.
Bwana Malema amesema tayari Serikali imechukua juhudi za awali
kukabiliana na mdudu huyo ikiwa ni pamoja na kutoa elimu kwa wananchi juu ya
utambuzi wa mdudu huyo kwa kuwataka Wananchi kung’oa mazao na kuyachoma pindi
wanapobaini uwepo wa mdudu huyo.
Pia tayari dawa tatu zimepitishwa na Wizara ya Kilimo Mifugo na Uvuvi
kupitia Taasisi ya uchunguzi wa Viatilifu (TPRI) zinazoangamiza wadudu hao
ambazo ni Duduba 450, Mupacrone 500 EC na Match Save kutoka Kampuni ya Syngenta
hivyo Wananchi wametakiwa kuzitumia haraka pindi wanapoona dalili za kuwepo wa
wadudu hao shambani.
Bwana Malema amesema kuwa katika kipindi cha miaka mingi Tanzania
imekuwa ikikumbwa na viwavijeshi aina ya African Armywarms ambapo mara zote
imekuwa ikiwadhibiti wadudu hao wanapojitokeza kwa kuwapa kiuatilifu
kinachosababaisha matumbo ya wadudu hao kujaa na hatimaye kuwasababishia vifo.
Ameongeza kuwa kwa mara ya kwanza Wizara ilipata taarifa ya uvamizi
katika shamba la Mwekezaji mkubwa Wilayani Nkasi Mkoani Rukwa mwezi Machi 2017
na walipofuatilia na kupeleka sampuli maabara mdudu huyo alibainika kwa jina la
Spodoptera frugiperda au Fall arymworm ambaye ni hatari na amekuwa akiripotiwa
katika maeneo mbalimbali duniani.
Kutokana na unyeti wa suala hilo Wizara ya Kilimo imewasiliana na
Shirika la Chakula Duniani (FAO), kwa ajili ya kuunganisha juhudi za pamoja ili
kumdhibiti mdudu huyo kabla hajasambaa kwenye maeneo mengi nchini.
No comments:
Post a Comment