A great place to access the latest news and information.

Breaking

Post Top Ad

Your Ad Spot

Sunday, March 13, 2022

DC Kanali Mwakisu: Atakayekwamisha anuani za makazi Kasulu kukiona

MKUU wa Wilaya ya Kasulu mkoani Kigoma, Kanali Isack Mwakisu amewatahadharisha wakazi wa Wilaya ya Kasulu mkoani Kigoma kuepuka vitendo vyovyote vinavyoweza kukwamisha zoezi la anuani za makazi.

Kauli hiyo ameitoa katika kikao kilichowahusisha viongozi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wa mkoa wa Kigoma walipokuwa wakihitimisha ziara ya siku mbili wilayani Kasulu.
Kanali Mwakisu ametoa kauli hiyo kufuatia baadhi ya hoja zilizowasilishwa katika kikao hicho kuhusu migogoro ya mipaka iliyopo katika vijiji na mitaa ya Wilaya ya Kasulu.

Amesema kuwa, mipaka hiyo kamwe isihusishwe na anuani za makazi na atakaposikia kuna mtu yeyote katika wilaya hiyo amesababisha kukwama kwa zoezi la anuani za makazi, atamchukulia hatua kali ikiwa ni pamoja na kumweka ndani.

"Rais wetu amekwishatoa pesa nyingi kwa ajili ya utekelezaji wa zoezi la anuani za makazi, sipo tayari kusikia kuwa kuna mtu anakwamisha zoezi hilo,"amesema.

Akizungumzia suala la wakimbizi wanaoingia nchini bila utaratibu, amewatala wakazi wa Wilaya ya Kasulu kushirikiana na serikali katika kukabiliana na tatizo hilo badala ya kuitegemea Idara ya Uhamiaji na vyombo vya usalama pekee kwa kuwa jukumu la ulinzi na usalama wa nchi ni la kila raia.

Ameongeza pia kuwa, tatizo la wahamiaji kutoka nchi jirani ni moja ya matatizo makubwa yaliyopo katika Wilaya ya Kasulu hivyo vyombo vya ulinzi pekee havitaweza kutokana na ukubwa wa tatizo hilo.

Awali katika kikao hicho, Katibu wa Chama Cha Mapinduzi wa mkoa wa Kigoma Mobutu Malima, amewaasa wataalamu na viongozi wa siasa Wilayani Kasulu kushirikiana kwa pamoja katika kutekeleza ilani ya Chama cha Mapinduzi.

Amesema kuwa, kazi ya viongozi wa Chama ni kuhakikisha kuwa ilani ya Chama inatekelezwa na kazi ya wataalamu ni kutekeleza ilani ya Chama.

Aidha, Malima ambaye ziara hiyo ni ziara yake ya kwanza Wilayani Kasulu tangu ateuliwe kushika wadhifa huo mwishoni mwa mwaka jana, ametoa pongezi kwa viongozi wa Wilaya hiyo kwa kazi wanazofanya.

Kikao hicho kilichofanyika katika ukumbi wa halmashauri ya mji wa Kasulu, kimewakutanisha wataalamu na madiwani wa Halmashauri na mji wa Kasulu.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages