Mwenyekiti wa Bodi ya Mfuko wa Barabara (RFB), Joseph Haule |
BODI ya Mfuko wa Barabara imeziamuru
halmashauri saba nchini zilizotumia zaidi ya Sh milioni 359.5
zilizotolewa kwa ajili ya kujengea barabara, lakini zikazitumia kununua
madawati na kujengea maabara kuzirudisha mara moja katika mfuko huo.
Halmashauri hizo ni Karagwe Sh milioni
55.5, Kyerwa Sh milioni 36.8, Ushetu Sh milioni 15.7, Masasi Mji Sh
milioni 31.3, Nanyumbu Sh milioni 110.7, Kilolo Sh milioni 102.3 na
Songea ya Mji Sh milioni 7.3, na zinatakiwa kurudishwa fedha hizo kabla
ya Oktoba 30, mwaka huu. Hayo yalisemwa mjini Dodoma jana na Mwenyekiti
wa Bodi ya Mfuko wa Barabara (RFB), Joseph Haule wakati akiwasilisha
taarifa ya ukaguzi wa kiufundi na fedha kwa kazi za ujenzi na
matengenezo ya barabara na madaraja kwa mwaka wa fedha 2014/15 na
2015/16.
“Kwa zile halmashauri za wilaya
zilizotumia fedha za Mfuko wa Barabara kwa matumizi mengine kama vile
kutengenezea madawati na ujenzi wa maabara, wakaguzi wa halmashauri
husika wahakikishe zinarudisha haraka katika akaunti ya Mfuko wa
Barabara ya Dharura,” alisema Haule na kufafanua kuwa halmashauri hizo
zilikiuka Sheria ya Fedha ya Mwaka 2001, Sheria ya Manunuzi ya Umma ya
mwaka 2011 na Sheria ya Tozo za Barabara na Mafuta na Kanuni zake.
Pia kuna halmashauri ambazo zililipia
jumla ya Sh milioni 87.1 kwenye kazi hewa ambazo hazijafanyika ambazo ni
pamoja na Mtwara ambayo ililipa Sh milioni 46.2, Tanga Mjini Sh milioni
12.1, Monduli Sh milioni 6.6, na Moshi Sh milioni 12.2 nazo zinatakiwa
kulipa fedha hizo. Halmashauri ya Gairo ambayo miradi mingi
haijatekelezwa kadiri ya mikataba ya makubaliano, ilipewa nafasi ya
kufika mbele ya Bodi ya Mfuko, lakini ilichelewa kufika.
“Halmashauri ya Kalambo, mkandarasi wake
aliidhinisha malipo ya Sh milioni 15.4 ya kupima kifusi ambacho
hakijashindiliwa kinyume cha mkataba unaotaka kuidhinisha malipo kifusi
kilichoshindiliwa,” alisema na kubainisha kuwa Halmashauri ya Kakonko
ilihamisha Sh milioni 13.7 zilizokuwa zimetengwa kwa ajili ya mradi wa
matengenezo ya barabara na kutekelezea mradi mwingine, kinyume cha
mkataba wa makubaliano. "Halmashauri ya Kondoa ilipewa zaidi ya Sh
milioni 60 kwa ajili ya kujenga maeneo korofi na ikajenga chini ya
kiwango na hivyo kuisababishia hasara kubwa serikali," alisema.
No comments:
Post a Comment