Kamati ya Ujenzi wa Ofisi 402 za Walimu kwa Mkoa wa Dar es
Salaam imepokea msaada wa matofali 1000 kutoka kwa kampuni ya A and Bel Impex
Tanzania Limited kwa ajili ya ujenzi wa ofisi za walimu wilaya ya Kigamboni.
Akizungumza
jijini Dar es Salaam Afisa Elimu Mkoa wa Dar es Salaam Hamis Lissu amesema
wanaipongeza kampuni hiyo kwa kujitolea msaada huo huku akieleza kuwa utasaidia
katika kuboresha elimu kwa ujenzi wa ofisi za walimu kwani katika
shule 513 za Mkoa wa Dar es Salaam asilimia kubwa ya takribani shule zaidi
ya 400 hazina ofisi za walimu jambo ambalo ni changamoto katika maendeleo ya
elimu.
Lissu amesema
kuwa ujenzi wa ofisi 402 za walimu kwa Mkoa wa Dar es Salaam utakamilika
kwa muda wa miaka miwili ila utakuwa na awamu katika shule za kila wilaya
ambapo ameelekeza matofali hayo 1000 yapelekwe shule ya Nguva Sekondari ya
Wilaya hiyo ya Kigamboni na ujenzi uanze mara moja kuanzia hivi sasa.
Kwa upande
wake Mkurugenzi wa kampuni ya A and Bel Impex Tanzania Limited iliyotoa
msaada wa matofali hayo bwana Thobias Hima ameeleza kuwa wameamua kuunga mkono
jitihada za Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Paul Makonda katika ujenzi wa ofisi
za walimu na watahakikisha pale panapohitajika msaada wanafanya hivyo kwa
maendeleo ya watanzania wote.
"Licha
ya kutoa matofali haya 1000 tumetoa pia na mashine ya kufyatulia matofali na
eneo la kufanyia shughuli hiyo la Mwembe Mdogo, Mtaa wa Minondo Kata ya
Somangila" Alisema.
Kwa upande
wake Mwenyekiti wa Kamati ya Ujenzi wa Ofisi 402 za Walimu Kanali Charles
Mbuge ameeleza kuwa ufyatuaji wa matofali utakuwa unafanyika majira ya usiku
katika eneo hila la kata ya Somangila, huku akihimiza wadau mbalimbali kuwaunga
mkono katika kufikia lengo la ujenzi wa ofisi hizo.
Kwa upande
wake Kaimu Mkurugenzi wa Manispaa ya Kigamboni David Mgonja ameeleza kuwa shule
zitakazo pitiwa na mpango huo ni 12 na zitakuwa kwa awamu huku 4 zikiwa za
sekondari na 8 za msingi, ambapo awamu ya kwanza itajumuisha shule mbili za
sekondari na tatu za msingi, za sekondari zikiwa Nguva na Tungi, huku za msingi
ni Mwongozo, Mizimbini na Vumilia Ukooni.
Afisa Elimu Mkoa wa Dar es Salaam Hamis Lissu akizungumza na waandishi wa habari alipokwenda kupokea matofali hayo.
Mwenyekiti wa kamati ya ujenzi wa ofisi 402 za walimu Mkoa wa Dar es Salaam, Kanali Charles Mbuge, akizungumza na baadhi ya wajumbe wa kamati ya ujenzi huo katika hafla hiyo.
Mkurugenzi wa kampuni ya A and Bel Impex Tanzania Limited ,Thobias Hima wa pili (kushoto) akizungumza na waandishi wa habari mara baada yakukabidhi matofali hayo. wengine ni wanakamati wa ujenzi wa ofisi za walimu.
No comments:
Post a Comment