Maelfu ya Wanawake waliotelekezwa na waume zao na hawapatiwi fedha ya matunzo ya Mtoto leo wamefurika kwenye ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam Mhe. Paul Makonda kwaajili ya kupatiwa Msaada wa kisheria chini ya wataalamu makini wakiwemo wanasheria, maafisa ustawi wa jamii, Jeshi la Polisi Dawati Jinsia na Ofisi ya Mkemia mkuu wa serikali.
Akizungumza na kinamama hao Makonda amesema Zoezi hilo litaendeshwa kwa muda wa siku tano ilikuhakikisha kila mwanamke anaefika ofisini kwake anasikilizwa kwa umakini na mwisho wa siku atendewe haki pasipo kuvunja Sheria.
Amesema ongezeko la Watoto wa Mitaani, Wizi,Utoaji Mimba, Mmomonyoko wa maadili na ugonjwa wa Ukimwi ni matokeo ya kutetereka kwa misingi ya familia hivyo ameamua kuanzisha zoezi hilo kwa lengo la kujenga Taifa bora.
Aidha Makonda amesema atahakikisha Mwanaume yoyote aliemzalisha mwanamke na kumtelekeza anatafutwa popote alipo ili aweze kutoa matunzo ya mtoto ili mwisho wa siku mtoto afurahie fursa ya Elimu Bure ambayo Rais Magufuli ameianzisha kwa lengo la kujenga taifa la kesho.
"Watoto hawa tunawategemea ili kujenga taifa la kesho tusipowajengea misingi imara hawataweza kufika kwani hata mafanikio yetu yanategemea kutoka kwa watoto"Amesema.
Pamoja na hayo Makonda amewataka pia Wanaume walioachiwa watoto wafike ofisini kwake ili wapatiwe msaada wa kisheria.
No comments:
Post a Comment