RAIS Pierre Nkurunziza wa Burundi
ametembelea maonesho ya kwanza ya biashara ya Tanzania nchini Burundi
yanayolenga kuangalia soko pana la bidhaa zinazotengenezwa na
wajasiriamali kutoka Tanzania na kusifu ubora wa bidhaa hizo.
Maonesho hayo yaliyofanyika katika
viwanja vya Tempete vilivyopo jijini Bujumbura, yalianza Septemba 28,
mwaka huu na yalitarajiwa kukamilika jana, yameandaliwa na Mamlaka ya
Maendeleo ya Biashara Tanzania (TanTrade) kwa kushirikiana na Mamlaka ya
Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) kwa lengo la kuongeza fursa za
kibiashara katika nchi za ukanda huu wa Afrika Mashariki na Kati.
“Hii ni ishara ya kukomaa kwa udugu kati
ya Tanzania na Burundi, wananchi wa Burundi walikuwa wakisafiri umbali
mrefu kufuata bidhaa hadi Dar es Salaam, lakini sasa wameletewa
mlangoni.
Kwa muda mrefu tumekuwa tukifurahia
bidhaa aina hii, lakini bei zilikuwa kubwa kutokana na gharama za
usafiri, kwa sasa mambo yamekuwa mazuri,” alisema Rais Nkurunziza. Rais
Nkurunziza aliongeza kuwa: “Uhusiano wetu unazidi kuimarika, naamini ile
dhana ya utangamano wa Jumuiya ya Afrika Mashariki inatekelezwa
kivitendo. Naahidi kuunga mkono juhudi zote za kuimarika kiuchumi kati
ya nchi mbili hizi.”
Ubalozi wa Tanzania nchini Burundi kwa
kiasi kikubwa umeshiriki kufanikisha maonesho haya chini ya Balozi
Rajabu Gamaha ambaye ndiye aliyewashawishi maofisa wa TanTrade kuwa na
maonesho aina hiyo kutokana na maombi ya kupata bidhaa kutoka Tanzania
kuwa mengi ofisini kwake. Awali katika hotuba yake ya ufunguzi Septemba
27, mwaka huu, Makamu wa Pili wa Rais wa Burundi, Dk Joseph Bitore
alisema biashara ni kitu kinachounganisha mataifa mawili kiuchumi hivyo
watachukulia maonesho hayo kujifunza, lakini pia kutanua wigo wa
mahusiano ya kiuchumi kati ya Tanzania na Burundi.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Bodi ya
Wakurugenzi TanTrade, Christopher Chiza alisema uamuzi wa kupeleka
bidhaa Burundi ulipofika mezani kwake hakutaka kusita kwa sababu alijua
hiyo ni njia pekee ya kufikisha mbali bidhaa za Kitanzania.
“Tunapofanikiwa kufika Burundi maana yake tunalenga soko pana la ukanda
huu, tunatarajia kufikia soko la Mashariki ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya
Congo kwa sababu hata wao tumearifiwa kuwa wananunua bidhaa kutoka
Burundi,” alisema Chiza.
Naye Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TanTrade,
Edwin Rutageruka aliahidi kuendeleza biashara kati ya Tanzania na
Burundi hata baada ya kumalizika kwa maonesho hayo. “Huu ni mwanzo,
tayari wafanyabiashara tulioongozana nao wamechukua mawasiliano ya
wateja wao na watawauliza wanahitaji nini ili walete.
No comments:
Post a Comment