PICHA NA MATUKIO MBALIMBALI
Mke
wa Rais Mama Janeth Magufuli leo ameongoza maelfu ya wanawake wa mkoa wa Dar es
salaam kuadhimisha kilele cha Siku ya Wanawake Duniani huku akiziomba asasi za
kiraia, na watu binafsi kushirikiana na serikali kuwapatia kinamama mbinu
mbalimbali, mafunzo, mitaji na kuwatafutia masoko ya bidhaa zao.
Mama
Magufuli pia ameupongeza mkoa wa Dar es salaam kwa kuanzisha vikundi zaidi ya
400 vya wanawake vinavyojishughulisha na shughuli mbali mbali ikiwemo
usindikaji mazao, ushonaji, uchoraji na kadhalika, pamoja na kuwa na vikundi
vya kukopeshana (VICOBA) vipatavyo 2,748 ambavyo kwa pamoja vina mtaji wa jumla
ya shilingi bilioni 10.78.
"Ni
imani yangu kuwa kama mikoa yote na taasisi nyingine za kiserikali na kiraia
zitaiga mfano wa Dar es salaam katika kuwawezesha wanawake kiuchumi pamoja na
kuwashirikisha kwenye shughuli za ujenzi wa viwanda basi tutawawezesha wanawake
kiuchumi ikiwemo kushiriki kwenye shughuli za ujenzi wa viwanda", alisema
Mama Magufuli amesema kwenye sherehe hizo zilizofanyika ukumbi wa Mlimani City.
Huku
akishangiliwa kwa nguvu, Mama Magufuli amesema japokuwa serikali inajitahidi
sana kuweka usawa wa jinsia na kuwawezesha wanawake kisiasa, kiuchumi, elimu na
afya, serikali peke yake haiwezi kuzimaliza changamoto zote, hivyo ni lazima
wananchi wenyewe washiriki katika kusukuma mbele gurudumu la maendeleo.
Mama
Magufuli amewapongeza viongozi wa awamu zote za nchi, ikiwa ni pamoja na
kinamama shupavu wa TANU na ASP na baadaye CCM ambao kwa namna moja ama
nyingine wameshiriki katika harakati za kumkomboa mwanamke nchini.
"Kutokana
na umuhimu wa siku ya leo naomba nitambue mchango wa Mama Maria Nyerere, Mama
Fatma Karume, Bibi Titi Mohamed, Mama Sophia Kawawa, Bi. Hadija Jabir, Bi
Johari Yusuf Akida, Mwajuma Koja, Bi. Mtumwa Fikirini na wengineo wengi. Hatuna
budi kuwapongeza sana akinamama hawa kwa kupigania haki za wanawake
nchini" alisema.
Mama
Magufuli ametanabahisha kwamba japokuwa vitendo vya unyanyasaji, dhuluma na
ukatili dhidi ya wanawake bado vinaendelea kwenye baadhi ya maeneo nchini,
Tanzania imepiga hatua kubwa na ni miongoni mwa nchi zinazosifika
duniani kwa kulinda na kusimamia haki na maslahi ya wanawake.
"Hivyo
basi hatuna budi kuwapongeza wote walioshiriki katika kulinda na kutetea haki
na maslahi ya wanawake nchini", alisema, kabla ya kutembelea maonesho ya
wajasiriamali kinamama waliopanga bidhaa zao katika kila pembe ya ukumbi huo.
Sherehe
hizo zilihudhuriwa pia na Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam Mhe. Paul Makonda
pamoja na wakuu wa Wilaya za Kinodnoni na Ilala, Mhe. Kisare Makori na Bi.
Sophia Mjema.
No comments:
Post a Comment