A great place to access the latest news and information.

Breaking

Post Top Ad

Your Ad Spot

Tuesday, December 19, 2017

OFISI YA MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI YAZINDUA BARAZA LA WAFANYAKAZI

  Mwanasheria Mkuu wa Serikali  Mhe. George Masaju  na  Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi wa Ofisi ya  Mwanasheria Mkuu akimkaribisha Mhe Waziri wa Katiba na Sheria  kuzindua Baraza  la Wafanyakazi na katika salamu zake alisema ni muhumu kwa Serikali  kuendelea kuiimarisha Ofisi ya Mwanasheria Mkuu kutokana na   umuhimu wake  katika maendeleo ya nchi, kiuchumi, kiusalama, katika utawala wa sheria na katiba
 Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Profesa Paramagamba Kabudi akitabasamu mara baada ya kufungua Baraza la Wafanyakazi wa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali  siku ya jumatatu. Baraza hilo linakutana kwa siku mbili katika ukumbi wa LAPF mkoani Dodoma.
 Wajumbe wa Baraza Kuu la Wafanyakazi wa Ofisi ya  Mwanasheria Mkuu wa Serikali wakiimba wimbo wa mshikamano wakati wa ufunguzi wa Baraza hilo, wajumbe wa   Baraza ni pamoja na  Mawakili  Wafawidhi wa Serikali, Wakuu wa Divisheni na Vitengo, Wajumbe wa TUGHE na mada mbalimbali zilitolewa wakati wa uzinduzi hao.



Mwanasheria Mkuu wa Serikali  Mhe. George Masaju amesema,  kutokana na mchango mkubwa wa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu katika maendeleo ya  kiuchumi, usalama, utawala wa sheria na utawala bora, Kuna   umuhimu wa Serikali kuendelea kuiimarisha Ofisi  hiyo.

Ameyasema hayo  wakati akimkaribisha Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe Profesa Palamagamba Kabudi kuzindua Baraza la  Wafanyakazi wa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali. Uzinduzi wa  baraza hilo  umefanyika siku ya jumatatu katika ukumbi wa mikutano wa Jengo la LAPF  Mkoani Dodoma.

Uzinduzi wa Baraza hilo,  ulitanguliwa  na  uchaguzi wa Katibu na Katibu Msaidizi.  Zoezi la uchaguzi lilisimamiwa na  Katibu Mkuu wa TUGHE Mkoa wa Dodoma Bw. John Mchenya,  Naibu Katibu Mkuu TUGHE Taifa Bi. Jane Mbura na  Afisa Kazi Bi. Razina Tuusa.  Waliochaguliwa kwa kura  za  Siri ni  Wakili wa Serikali Mkuu Monica Mbono ambaye anakuwa  Katibu na  Bw. Michael Masanja anakuwa  Katibu msaidizi.

Mhe. Masaju  akiwa ni  Mwenyekiti wa Baraza la wafanyakazi, ameyataja maeneo ambayo  Serikali  inatakiwa kuendelea kuyaimarisha katika Ofisi ya Mwanasheria Mkuu ni pamoja na,  Raslimali fedha, mafunzo, makazi salama kwaajli ya  mawakili wa serikali na  miundombinu ya ofisi.

“Mhe. Waziri, yapo masuala ya kisera ambayo tunaomba  Serikali  inayashughulikie  ipasavyo ili kuiwezesha Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kuendelea kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi. Maeneo hayo ni  kuajiri Mawakili wa Serikali na Watumishi wa Kada zingine, kujenga majengo ya Ofisi ya Mwanasheria Mkuu  katika Ofisi  za Wilaya na Mikoa ili  kuokoa fedha inayotumika kulipia pango”. Ameleza Mwanasheria Mkuu.

Kwa upande wa mafunzo,  Mwanasheria Mkuu, ameishauri Serikali  katika  kuwajengea uwezo wa kitaalam Mawakili wa Serikali na  watumishi wenzao katika maeneo ya kipaumbele na kuimarisha maslahi ya mawakili wa serikali na watumishi wote katika Ofisi ya  Mwanasheria  Mkuu wa Serikali.

Pamoja na kutaja changamoto mbalimbali ambazo Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali imekuwa ikikabiliana nazo katika utekelezaji wa Majukumu yake. Mwanasheria Mkuu  ametaja mafanikio ambayo Ofisi imeyapata katika utekelezaji wa  majukumu yake.

Baadhi ya mafanikio hayo ni  pamoja na kuokoa fedha nyingi na kuingiza serikalini mapato kupitia uendeshaji wa mashtaka na mashauri mbalimbali mahakamani na katika  mabaraza ya usuluhishi, ushiriki katika majadiliano ya Mikataba na uhakiki wake na kudumisha utawala wa sheria na  utengamano nchini.

Mafanikio mengine ni  pamoja na  kuingiza serikalini kiazi cha shilingi  1.039 Bilioni iliyotokana na faini  baada ya  serikali kushinda kesi 110 zinazohusiana na makosa chini ya sheria ya  uhifadhi wa wanyamapori ya mwaka 2009.

 Mafanikio mengine ni urejeshwaji wa mali zilizopatikana  kwa njia ya uhalifu  ambapo kesi 10 zilitolewa uamuzi na mali zenye thamani  ya zaidi ya   Bilioni  2  zilitaifishwa.  Vile vile    Serikali ilishinda kesi 3 zinazohusiana na utakatishaji wa fedha haramu ambapo mbali na watuhumiwa kutiwa hatiani  kiasi cha fedha kipatacho shilingi milioni 29,439,452 kilitaifishwa.

Mwanasheria Mkuu wa Serikali akifafanua zaidi mafanikio yanayotokana na  majukumu ya Ofisi yake kuwa ni  yale  yanayotokana na mashauri mawili yanayohusu  kuingiza nchini magari mawili ya kifahari yaliyotolewa uamuzi kwa watuhumiwa kupatikana na hatia na magari  hayo ambayo  thamani yake ni shilingi bilioni 1.7 yalitaifishwa kuwa mali ya serikali na fidia ya shilingi milioni 200 kulipwa serikalini.

Akizindua  Baraza la wafanyakazi wa Ofisi ya Mwanasheria  Mkuu, Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe.Profesa Palamagamba Kabudi alipongeza uamuzi wa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu  kuzindua Baraza lake na kukutana kwa siku mbili kujadili masuala mbalimbali.

Kwa mujibu wa  Waziri Kabudi, Baraza la Wafanyakazi ni chombo cha kupanga   mipango muhimu na kuhakikisha kuwa kinafanyika pia katika kutathmini  ambacho Ofisi imepanga kukifanya na  kimefanyika  kwa kiwango gani.

Akasema “sote tu mashahidi kuwa tangu  Serikali ya Awamu ya  Tano iingie madarakani  msisitizo umekuwa kwa kila taasisi kuongeza ufanisi katika kutekeleza majukumu yake. Awamu hii inasisitiza watumishi na taasisi kuondokana na tabia ya kufanya kazi kwa mazoea na kuhakikisha utendaji wao  unaleta tija katika serikali” ameeleza Waziri

Na akalitaka Baraza hilo la wafanyakazi kutathimini ni jinsi gani  linaishauri serikali na taasisi zake katika masuala yote kwa kuhakikisha kwamba ushauri unaotolewa unabeba maslahi mapaba ya taifa na kuzingatia vipaumbele vya serikali ya awamu ya tano

Akasisitiza pia kwamba tathmini hiyo inatakiwa kwenda mbali zaidi kwa kujiuliza kama m Miswada inayoadaliwa inakidhi vigezo vya kitaalam, je inabeba maslahi mapana ya nchi, au je jukumu la kuiwakilisha Serikali mahakamani liinatekelezwa kwa kiwango gani cha ufanini, je kesi na mashauri yote yanasimamiwa na kuendeshwa kwa weledi na uzalendo na ni kwa kiasi gani uratibu wa upelepezi na uendeshaji wa mashauri unafanyika kwa weledi na umakini.

Baraza la Wafanyakazi wa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali  linahudhuriwa na  Mwanasheria Mkuu wa Serikali  ambaye ni  Mwenyekiti wa Baraza,  naibu Mwanasheria Mkuu, Bw. Gerson Mdemu ambaye pia ni Makamu Mwenyekiti , Mkurugenzi wa Mashtaka, Bw. Biswalo Maganga, Mawakili  Wafadhiwi kutoka Mikoa yote na  Wilaya ambako kuna Ofisi  za Mwanasheria Mkuu wa Serikali,   Wakuu wa Divisheni na  Vitengo na  Na wajumbe wa TUGHE.

Aidha mada mbalimbali zinatolewa zikiwamo zinazohusu maadili katika utumishi wa umma na utunzaji wa siri za serikali.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages